Latest Stories

TOP 5 Most Popular Post

Recently Comments

FFFFFFFFFFFFF

FFFFFFFFFFFFF
XXXXXXXXXXX

FFFFFFFFFFFFF

FFFFFFFFFFFFF
XXXXXXXXXXX

Dk Mwakyembe 'avamia' mabasi Ubungo alfajiri 0 Comments

By Unknown
Tuesday, July 10, 2012 | Posted in ,

WAZIRI wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe, ameibuka ghafla katika Kituo Kikuu cha Mabasi cha Ubungo (UBT), Dar es Salaam na kufanya ukaguzi wa nauli za abiria wa kwenda mikoani na kusimamia waliolanguliwa kurejeshewa fedha.

Dk Mwakyembe aliyefika kituoni hapo jana saa 11.30 alfajiri na kuingia katika mabasi, moja baada ya lingine, kukagua tiketi kwa abiria pia alisimamia kutozwa faini kwa baadhi ya mabasi kuanzia Sh 250, 000 hadi Sh 750,000 kulingana na idadi ya makosa waliyokutwa nayo.
Pia aliwaagiza watendaji wakuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (SUMATRA), kufanya kazi ya ukaguzi kituoni hapo kwa miezi mitatu mfululizo ili kuondoa matatizo yaliyopo.
“Nawataka sasa wote mwache kukaa ofisini, mtoke nje kufanya ukaguzi, muda huu nilipaswa kuwa bungeni Dodoma, lakini kazi mliyopaswa kufanya nyie mimi nawajibika kuifanya, kuanzia sasa nataka kuona kila mtu anafanya kazi yake kikamilifu,” alisema Dk Mwakyembe.
Alianza ukaguzi huo kimyakimya katika basi la Green Star na kuendelea katika basi la Musoma Express, huku akifuatana na Kaimu Mkurugenzi wa Sumatra, Ahmad Kilima, watendaji wake na maofisa wa Polisi.
Udanganyifu nauli Katika ukaguzi huo aliofanya zaidi katika mabasi yanayokwenda mikoa ya Mwanza, Mbeya, Musoma na Arusha, Mwakyembe alibaini udanganyifu katika nauli ambapo abiria walikuwa wakitozwa kiasi kikubwa tofauti na viwango vya Serikali.
Mabasi yaliyofanyiwa ukaguzi na kukutwa yakitoza nauli hizo ni Sumry, Najimunisa, Musoma Express, ‘RS Bus’, Princess Shabaha, Buffalo na Best Line.
Mwakyembe aliyekuwa amesimama katika lango la kutokea mabasi kituoni hapo, aliagiza kusimamishwa kwa kila basi lililokuwa likitoka na kuingia kuhoji abiria nauli waliyotozwa kwa kila sehemu wanayokwenda, huku akitaka uthibitisho kwa maofisa wa Sumatra aliokuwa nao.
“Tunashukuru Waziri kwa kuja kujionea hali halisi, ukweli sisi abiria tunanyanyasika, wamiliki wengi wa mabasi haya wanapandisha nauli bila kufuata utaratibu, ujio wako tunaamini utasaidia kuondoa tatizo hili,” alisikika abiria ndani ya basi la RS, lililokuwa likienda Bukoba huku akiungwa mkono na wenzake.
Katika ukaguzi huo, Dk Mwakyembe alibaini kuwapo abiria waliotozwa Sh 60,000 kwa safari ya Bukoba tofauti na nauli halali ya Sh 51,000 katika basi la hadhi ya anasa.
Wapo pia abiria wa Mwanza waliokutwa wametozwa nauli ya hadi Sh 45,000 kwa safari hiyo tofauti na Sh 35,000 ya Sumatra.
Abiria wa Singida, walitozwa nauli ya Sh 28,000 hadi Sh 38,000 wakati halali ni Sh 21,000. Kukosa dereva wa ziada Mbali na masuala ya nauli, pia Dk Mwakyembe alisimamia utozaji faini kwa mabasi yaliyobainika kuwa na dereva mmoja na kusema yamekuwa chanzo cha ajali nyingi zinazosababishwa na uzembe wa madereva.
“Ajali nyingi zinazoendelea kutokea nchini kwa asilimia 75 zinasababishwa na uzembe wa madereva, hatutaki kuona maisha ya Watanzania yakiendelea kupotea kwa uzembe huu,” alisema Dk Mwakyembe ambaye jana mchana alitarajia kukutana na viongozi wa Sumatra na wadau wa sekta hiyo kwa ajili ya mazungumzo.
Kaimu Mkurugenzi wa Sumatra, Ahmad Kilima, alisema sasa wanajipanga kufanya kazi hiyo kwa nguvu zote, ili kubaini wamiliki wa mabasi wanaoendelea kuvunja utaratibu wa usafirishaji kwa makusudi.
Alisema ufinyu wa wafanyakazi wa ofisi hiyo kwa kiwango kikubwa ndio uliosababisha kufanyika kwa ukaguzi wa kusuasua, hivyo wanajipanga kuongeza wafanyakazi ili kuimarisha ukaguzi.
Hatua ya Dk Mwakyembe kutembelea kituo hicho ni mwendelezo wa utaratibu aliojiwekea tangu alipoteuliwa kushika nafasi hiyo na tayari amefanya ukaguzi wa ghafla katika Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara), Shirika la Reli (TRL) na Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL). Pia ni Waziri pekee ambaye hivi karibuni alisafiri kwa treni Reli ya Kati kutoka Dar es Salaam kwenda Dodoma kuhudhuria mkutano unaoendelea wa Bunge la Bajeti, ambapo pamoja na mambo mengine alikagua ubora wa mabehewa na utendaji kazi.

Follow any responses to the RSS 2.0. Leave a response

Leave a reply

0 comments for "Dk Mwakyembe 'avamia' mabasi Ubungo alfajiri"